Sababu 10 za kwa nini tunasherehekea Uhuru
wetu. Hii ni sehemu ya hotuba niliyoitoa kwa Watanzania wanaoishi
majimbo ya DMV Marekani juzi Jumamosi katika hafla ya kuadhimisha siku
ya Uhuru.
1) Uhuru wetu bado upo, haujapotea. Japo leo hii
Tanganyika haipo tena, bado tuna haki ya kusherehekea siku tulipopata
Uhuru kwavile mpaka leo Uhuru huo tunao. Tuna mamlaka kamili na
tunajitawala wenyewe tofauti na iliyokuwa awali. Katiba ya Tanzania
niliyoitaja katika kifungu chake cha 151(1) kinafafanua kuhusu “Tanzania
Bara” kuwa ni “eneo lote la Jamhuri ya Muungano ambalo zamani ilikuwa
eneo la Jamhuri ya Tanganyika.” Kwa maana nyingine, japo jina la
Tanganyika halitumiki tena, eneo lake bado lipo, watu wake bado wapo,
mamlaka yake na Uhuru wake umezingatiwa na unatambulika ndani ya Katiba
ya sasa. Kutokuwapo kwa Tanganyika ni kwa jina tu!
2)
Tunasherehekea kwavile kuwapo kwa Tanzania Bara kunapelekea kuwapo kwa
NCHI ya Tanzania (kama jinsi Mapinduzi ya Zanzibar, ambayo mwakani
tutasherehekea Miaka 50, vile vile yanapelekea kuwapo kwa nchi ya
Tanzania).
3) Tunasherehekea Uhuru kama sehemu ya kuutambua
UTAIFA wetu wa Tanzania. Uhuru wetu ndio unaotambulisha Taifa letu.
Wakati wa kupata Uhuru ndipo tulipopata mamlaka kamili, bendera, nembo,
mipaka na pia tulitambulika na wenzetu duniani kwamba sisi ni Taifa.
4) Tunasherehekea Uhuru wetu kama njia ya kukumbushana kuhusu haja ya kuendelea kuulinda Uhuru wetu.
5) Tunasherehekea Uhuru wetu kama njia ya kukumbushana kuhusu haja
ya kuendelea kuulinda Muungano wetu, kwa vile bila ya Uhuru (na
Mapinduzi Zanzibar) tusingekuwa na Muungano.
6)
Tunasherehekea Uhuru wetu kwavile tuna haja pia ya kuwaenzi wale
waliopigania Uhuru wetu kwa vile walifanya kazi kubwa, wengi walifungwa,
wengi walipoteza mali zao na maisha yao ili sisi tuwe Huru.
7)
Tunasherehekea Uhuru wetu ili kukumbushana kwamba kazi ya kuijenga
nchi yetu bado haijaisha. January alisema kwamba viongozi waliopigania
Uhuru wetu walianza pia kazi ya kujenga Taifa letu kwa kutuunganisha
katika makabila, katika dini n.k. Zikafanyika jitihadi nyingi na za
makusudi za kuijenga nchi yetu ili iwe nchi moja ya watu wanaopendana,
wanaoheshimiana, wanaoaminiana, wanaoshirikiana, wanaofanya kazi kwa
pamoja katika kujenga Taifa. Hiyo kazi ya kujenga nchi yetu bado
haijaisha kwa vile bado kuna changamoto nyingi sana za maendeleo. Vile
vile, kuna changamoto mpya ambazo zimejitokeza zinazohatarisha Umoja wa
Taifa letu. Hizi ni zile nyufa alizotaja Mwalimu Nyerere kama vile
udini, ukabila, rushwa n.k. Kwahiyo Uhuru wetu upo hatarini sana kama
hatutajidhatiti kwa dhati kuhakikisha kwamba bado tunaendelea na kazi ya
ujenzi wa Taifa letu.
Kuthaminiwa Utu wetu. January alikumbusha kwamba hii ndiyo ilikuwa
sababu kubwa ya msingi kwanini wazee wetu walipigania kupata Uhuru.
Walitaka kuondokana na kudhalilishwa, kutawaliwa, kutumwa, kunyanyaswa,
kunyonywa na kuwa chini ya mtu mwingine kutoka sehemu nyingine. Mtu huyo
anakuja anakalia nchi yako halafu anakufanya wewe kuwa ni mtu wa daraja
la chini, kisha anakuamulia uishi vipi, anakuamulia lugha gani utumie,
anaamua watoto wako wasome nini n.k. Wakasema hapana, kila mtu anahaki
ya kuwa Huru na kuthaminiwa Utu wake, kujikomboa kwenye udhalimu na
kujitoa kwenye udhalilishaji.
9) Lengo la kupigania Uhuru
lilikuwa ili tupate uwezo wa Kujiamulia mambo yetu yenyewe ili
kutengeneze nchi ambayo tunaitaka sisi wenyewe. Lakini January aliweka
bayana kwamba Malengo ya Uhuru bado hatujayafikia yote. Na ndiyo kazi
ambayo sote tunapaswa kuifanya ili malengo hayo tuyafikie. Kila awamu ya
uongozi wa nchi yetu baada ya Uhuru imetusogeza hatua moja au kadhaa
kufikia Malengo ya Uhuru. Kikubwa ni kwamba bado tunayo kazi ya kujenga
uwezo wa kiuchumi na uwezo wa kiutawala ili kuondoa umaskini wa watu
wetu ili tuweze kufikia Malengo ya Uhuru wetu.
10) Pamoja na
changamoto zilizopo, ambazo alisema Serikali ya sasa chini ya Rais
Kikwete inazitambua na inaendelea kuzifanyia kazi, nchi yetu bado ni
nchi nzuri ya kuishi duniani. Hili pia ni jambo jema la kuherehekea
wakati wa maadhimisho ya Uhuru. Watanzania bado kwa kiasi kikubwa ni
wamoja, wanapendana na wanaheshimiana.
January alimaliza kwa
kusema, “Nchi yetu bado inaweza kuwa nzuri sana kuliko ilivyo sasa. Sisi
wenyewe tunaweza kuiharibu au kuijenga nchi yetu”.
No comments:
Post a Comment