Monday, December 09, 2013

HERI YA SIKUKUU YA UHURU - Miaka 52!

Ni kwa muda mrefu sasa nasikia, kuona na kusoma kwenye vyombo vya habari juu ya miaka kadhaa ya uhuru. Tarehe 9 Desemba mwaka huu, wapo wanaosema ni maadhimisho ya miaka 52 ya uhuru wa Tanzania, wengine wanasema miaka 52 ya uhuru wa Tanzania Bara, na wapo pia wanaosema miaka 52 ya uhuru wa Tanganyika. Swali la kwanza kunijia akilini,  kati ya hao wote ni wapi walio sahihi?
Nchi ya Tanganyika ilipata uhuru tarehe 9 Desemba mwaka 1961 na Mwalimu Julius Kambarage Nyerere akaapishwa kuwa waziri mkuu wa kwanza wa nchi huru hiyo. Tarehe kama hiyo ya mwezi Desemba mwaka 1962 Tanganyika ikawa jamhuri na hivyo kumfanya Mwalimu Nyerere kuapishwa kuwa rais wa kwanza wa Tanganyika.
Tarehe 26 Aprili mwaka 1964, baada ya Mapinduzi ya Zanzibar, Tanganyika ikaungana na Zanzibar kutengeneza nchi mpya inayoitwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.  Jamhuri hiyo ya Muungano inadumu hadi sasa. Siku hiyo Mwalimu Nyerere aliapishwa kuwa rais wa kwanza wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Siku hiyo pia nchi ya Tanganyika ilikufa rasmi.
Kwa hiyo tukisema kundi la kwanza la watu wanaosema tunasherehekea miaka 52 ya uhuru wa Tanzania ndio liko sahihi, tutakuwa kwanza tunajidanganya wenyewe, tunawadanganya wanetu, wajukuu zetu na ulimwengu mzima kwa kuwa nchi ya Tanzania inafikisha miaka 52 tarehe 26 Aprili mwaka 2016 kwa kuwa imezaliwa tarehe hiyo mwaka 1964. Lakini pia tutakuwa hatuwatendei haki Wazanzibari kwa kuwachanganya kwenye jambo lisilowahusu.

No comments:

Post a Comment